
Kipute cha – Over ‘40’ Football Tournament Mombasa ambacho kilitamatika jana kwa nyasi kuumia katika uga wa Serani kilivutia wadogo kwa wakubwa huku timu ya Wazee Health wakitwaa ubingwa wa ngarambe hiyo dhidi ya Ziwani Old Guard kwa mikwaju ya penati. [4 – 2]
Ni michuano iliochukua kipindi cha miezi miwili ikishirikisha timu 12 kutoka maeneo bunge yote sita kutoka kaunti ya Mombasa ikiwemo Fetuwe Fc iliyoridhika na nafasi ya tatu.
Wachezaji wakongwe waliotamba miaka ya nyuma kama Ali Breki aliyeichezea Harrambe Stars wakati mmoja walipamba makala ya kindumbwendumbwe hicho ambacho kilikuwa ukichengwa tulia.
Lengo zima la maandalizi hayo kutoka kwa wazee wazima kwa jumla lilikuwa kwao kukaa fiti kiafya na zaidi kuwapa vijana changamoto ya kuacha kusinzia bali kupiga zoezi pamoja na kujishugulisha na mambo yenye kuleta natija katika maisha yao ya kila siku.
Mwalimu Mwaguzo ambaye ni Jembe la kutegemewa kutoka upande wa Wazee Health akinyanyua kombe waliloshinda baada ya kuvishwa nishani za dhahabu alipongeza kila timu iliyoshiriki na wadau wote katika nafasi zao waolijitahidi kufanikisha michuano hiyo kwa jumla.